Vilevile amewakumbuka na kuwaenzi mashahidi na Imam Khomeini na kusema:
"Mwaka mpya ninaupa jina la Mwaka wa Uchumi Ngangari (kimuqawama), Hatua na Vitendo”.
Ayatullah
Khamenei ameashiria suala la kusadifiana siku ya kuzaliwa Bibi Fatima
Zahra (as) na mwanzo na mwisho mwaka mpya 1395 na kusema anatarajia kuwa
mwaka huu utakuwa mwaka wenye baraka kwa taifa la Iran na katika mwaka
huu tutaweza kupata darsa na somo kutokana na miongozo na maisha ya Bibi
huyo adhimu kwa kufaidika na masuala ya kiroho ya mtukufu huyo.
Matini kamili ya ujumbe huo ni kama ifuatavyo:
سم الله الرحمن الرحیم
یا مقلّب القلوب و الابصار، یا مدبّر اللّیل و النّهار، یا محوّل الحول و الاحوال، حوّل حالنا الی احسن الحال
Kwa jina la Allah Mwingi wa rehema Mwenye kurehemu
Ewe Mgeuzaji wa nyoyo na basari! Ewe Mpangiliaji wa Usiku na Mchana!
Ewe Mbadilishaji wa mwaka na hali! Badilisha hali zetu kuwa bora ya hali.
Assalaamu
alaa Swiddiqat at Twahirah, Faatimatu al Mardhiyyah binti wa Mtume wa
Mwenyezi Mungu, amani ya Allah iwe juu yake na Aal zake. Amani iwe juu
ya Waliyyullahil A'adham roho zetu ziwe fidia kwake na Mwenyezi Mungu
aharakishe faraja yake.
Ninaanza kutumia fursa hii kutoa mkono wa
baraka na fanaka kwa familia zote za Kiirani na Wairani walioko katika
kila kona ya dunia. Nakutakieni sikukuu iliyojaa baraka wananchi
wenzangu azizi. Mkono wangu wa baraka za idi uziendee hasa familia azizi
za mashahidi, majeruhi azizi wa kivita na familia zao na watu wote
wanaojitolea katika njia ya Mwenyezi Mungu na ninaitumia fursa hii
kuwakumbuka kwa wema mashahidi wetu watukufu na Imam wetu azizi.
Mwaka
huu mpya ulioanza hivi punde - mwaka 95 - (Hijria Shamsia) umepata
baraka za jina la Bibi Fatimatuz Zahra (Salamullahi Alayha) mwanzo wake
na mwisho wake. Mwanzo wake mwaka huu umesadifiana na maadhimisho ya
kukumbuka kuzaliwa mtukufu huyo kulingana na mwaka wa Hijria Qamaria na
mwisho wake pia itakuwa vivyo hivyo. Hivyo ni matumaini yetu Inshaallah
mwaka huu wa 1395 (Hijria Shamsia) utakuwa mwaka uliojaa baraka za Bibi
Fatimatuz Zahra kwa taifa la Iran na tutaweza kufaidika na kupata somo
la kimaanawi kutoka kwa mtukufu huyo, na kustafidi vizuri miongozo ya
busara ya mtukufu huyo na maisha ya mtukufu huyo.
Mwaka ulioisha -
mwaka 94 - kama ilivyokuwa kwa miaka mingine yote, uliandamana na mambo
matamu na machungu pamoja na panda shuka nyingi na hilo ni jambo la
kawaida katika maisha. Mwaka huo uliandamana na matukio machungu
kuanzisha lile la Mina, hadi matukio matamu kama maandamano makubwa ya
Bahman 22 (Februari 11, siku zinapofikia kileleni sherehe za Mapinduzi
ya Kiislamu ya nchini Iran) na hadi kwenye uchaguzi wa tarehe 7 Isfand
(Februari 26) na vile vile uzoefu wa JCPOA (makubaliano ya nyuklia baina
ya Iran na kundi la 5+1) na pia kuanzia kwenye matumaini yalijitokeza
hadi kwenye wasiwasi ulioambatana na jambo hilo. Yote hayo ni miongoni
mwa matukio ya mwaka huo, na hiyo ndiyo hali inavyokuwa katika miaka
yote.
Miaka na siku za maisha ya mwanadamu huandamana na fursa mbali
mbali na pia huwa na vitisho tofauti. Vipaji vyetu vinapaswa vionekane
kupitia kutumia vizuri fursa tunazopata na hata vitisho tunavyokumbana
navyo, ili kuvigeuza vitisho hivyo kuwa fursa nzuri kwetu. Hivi sasa
tumeingia kwenye mwaka 95. Katika mwaka huu, kama ilivyo mara zote,
zitakuweko fursa mbali mbali na vitisho pia. Kila mmoja wetu anapaswa
kufanya juhudi ya kuhakikisha tunatumia vizuri fursa tutakazopata mwaka
huu kwa maana halisi ya neno ili kuifanya nchi yetu ishuhudie tofauti za
waziwazi na miaka iliyopita, kuanzia mwanzo hadi mwisho wa mwaka huu.
Kuna
matumaini mbali mbali kuhusu mwaka huu wa 1395. Wakati mtu anapoangalia
hali na mambo mbali mbali, anapata matumaini mazuri. Tab'an, inabidi
juhudi zifanyike ili kufanikisha kivitendo matumaini hayo. Inabidi
kufanyike kazi za usiku na mchana na kufanyike jitihada za kila namna
bila ya kusita na wala kukwama sehemu yoyote ile katika juhudi za
kufanikisha matumaini hayo. Jambo hasa linalotakiwa ni kuwa, taifa la
Iran lihakikishe linafanya mambo ambayo yatalitoa katika hali ya
kuathiriwa na vitisho vya maadui na uadui wao. Tunapaswa tuhakikishe
kuwa tunajiwekea kinga madhubuti ambayo itatufanya tusidhuriwe na
vitisho vya maadui. Yaani tuhakikishe kuwa uwezekano wa kudhuriwa na
vitisho hivyo ni wa asilimia sifuri.
Ninavyoamini mimi ni kuwa,
suala la uchumi ndilo la kupewa kipaumbele cha kwanza kabisa. Yaani
wakati mtu anapoangalia masuala yenye vipaumbele anaona kuwa kati ya
vipaumbele vyote hivyo, suala la uchumi ndilo la haraka zaidi na la
karibu zaidi. Kama kwa taufiki ya Mwenyezi Mungu, wananchi na serikali
na viongozi wa sekta mbali mbali watafanikiwa kufanya kazi nzuri, kwa
njia sahihi na inavyotakiwa katika masuala ya kiuchumi, basi ni
matumaini yetu kuwa jambo hilo litaathiri pia katika masuala mengine
kama vile ya kijamii, kama vile matatizo ya kijamii, kama vile masuala
ya kimaadili na kama vile masuala ya kiutamaduni.
Jambo la muhimu na
la kimsingi katika suala la uchumi, ni suala la uzalishaji wa bidhaa za
ndani ya nchi; ni suala la kuandaa nafasi za kazi na kuondoa ukosefu wa
kazi; ni suala la kuimarisha na kusatawisha uchumi na kupambana na
uzorotaji wa kiuchumi; hayo ni masuala ambayo wanakabiliana nayo
wananchi; hivi ndivyo vitu ambavyo wananchi wanavihisi na wanavitaka na
hata takwimu na matamshi ya viongozi wenyewe nchini yanaonesha kuwa,
haya ndiyo matakwa ya wananchi na kwa kwa hakika matakwa hayo ni sahihi
na ni ya mahala pake kabisa.
Kama tunataka kutatua tatizo la kuzora
uchumi, na ili tuweze kutatua tatizo la uzalishaji wa bidhaa za ndani na
tutatue pia suala la ukosefu wa kazi, kama tutataka kudhibiti mambo
yote hayo, basi tujue kuwa utatuzi wa masuala yote hayo unapatikana
katika majimui ya muqawama wa kiuchumi na katika uchumi wa kimuqawama na
wa kusimama kidete. Uchumi wa kimuqawama unajumuisha mambo yote hayo.
Inawezekana kupambana na ukosefu wa kazi kupitia uchumi wa kimuqawama;
inawezekana kupambana na uzorotaji wa uchumi kwa kutumia uchumi wa
kimuqawama, kama ambavyo inawezekana pia kupambana na ughali wa maisha;
kukabiliana na vitisho vya maadui na kusimama kidete kupitia uchumi huo,
inawezekana kuiandalia nchi fursa nyingi na kuzitumia vizuri fursa hizo
kwa sharti kwamba tuufanyie kazi uchumi wa kimuqawama na tujitahidi
kuufanikisha kivitendo na inavyotakiwa.
Ripoti ambazo wamenipa ndugu
zetu serikalini zinaonesha kuwa wamefanya kazi kubwa, lakini yote hayo
ni utangulizi tu. Kazi za kuandaa miswada na ajenda za sekta tofauti;
hizo ni kazi za utangulizi tu; amma jambo la lazima hapa ni kuendelea
kwa kazi hizo, jambo la lazima ni kuchukuliwa hatua na kutekelezwa
kivitendo mambo hayo, ili wananchi waweze kuona matunda yake; hili ndilo
jukumu letu; na Inshaallah nitalitolea ufafanuzi zaidi suala hilo
wakati nitakapozungumza na wananchi wetu azizi wa matabaka tofauti.
Kwa
kuzingatia yote hayo nimeona nara na kaulimbiu yetu mwaka huu iwe ni
"Uchumi wa Kimuqawama, Hatua na Vitendo." Hii ni njia na baraste
iliyonyooka kuelekea kwenye kitu tulichokikusudia. Tab'an sitegemei kuwa
hatua na vitendo hivyo vitaweza kumaliza matatizo yote katika kipindi
cha mwaka mmoja; lakini nina yakini kwamba kama hatua na vitendo
vitafanyika kwa mpangililio mzuri na kwa utekelezaji sahihi, basi
matunda na athari ya jambo hilo tutaziona wazi wazi mwishoni mwa mwaka
huu. Ninawashukuru watu wote waliofanya juhudi na wanaoendelea kufanya
juhudi katika njia hii.
Kwa mara nyingine ninatuma salamu na baraka
zangu za idi kwa taifa letu azizi nikimuombea rehema na amani Mtume wetu
Muhammad na Aal Muhamad pamoja na Imam Mahdi (Amani za Mwenyezi Mungu
ziwe juu yake, na roho zetu ziwe fidia kwake).
Wassalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh.
3484210