Katika dikrii yake , Ayatullah Sayyed Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu ametoa shukrani zake za dhati kutokana na huduma ambazo zimetolewa na Majeshi ya Iran kwa wananchi katika uga wa vita dhidi ya corona na kuongeza kuwa kuna haja ya kuratibiwa huduma hizo chini ya usimamizi wa 'Kituo cha Afya na Matibabu' ili kuzuia kuenea zaidi ugonjwa huu.
Aidha Ayatullah Khamenei amesema: "Hatua hii ichukuliwe kwa kuzingatia dalili za kuwepo uwezekano wa 'hujuma ya kibiolojia' katika kadhia hii ya ugonjwa wa corona." Amesema hatua zitakazochukuliwa zinaweza kuwa na muelekeo wa mazoezi ya ulinzi wa kibiolojia ili kuimarisha nguvu na uwezo wa kitaifa.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa moja ya majukumu ya kituo hicho kitakachoundwa ni kugawa majukumu na kazi baina yai taasisi na vitengo mbali mbali vya Majeshi ya Iran. Aidha amesema Kituo cha Afya na Matibabu cha Majeshi ya Iran kinapaswa kushirikiana kikamilifu na serikali pamoja na Wizara ya Afya ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Ayatullah Khamenei ameelezea matumaini yake kuwa, kwa muongozo wa Mwenyezi Mungu SWT, na himaya ya salio la Mwenyezi Mungu kwenye ardhi, nyoyo zetu ziwe muhanga kwa ajili yake, taifa la Iran litaweza kupata ushindi na kupata usalama na afya.