Sayyed Hassan Nasrallah, Katibu Mkuu wa Hizbullah akizungumza Ijumaa usiku kwa kupitia televisheni ya Al Manar amesema Marekani imekuwa ikificha ukweli kuhusu idadi ya waliougua na waliofariki dunia kutokana na COVID-19 (kirusi cha corona) na kuongeza kuwa: "Trump na timu yake wamekuwa wakijaribu kupuuza hatari ya kirusi cha corona na taathira zake mbaya ndani ya Marekani."
Katibu Mkuu wa Hizbullah ameashiria madai ya wakuu wa Marekani kuwa wako tayari kuisaidia Iran kukabiliana na corona na kuongeza kuwa: "Iran haihitajii msaada wa Marekani katika kukabiliana na kirusi cha corona."
Nasrallah ameongeza kuwa, hatua pekee ambayo Marekani inapaswa kuchukua ni kuondoa vikwazo vyake vya kidhalimu dhidi ya Iran.
Sayyed Hassan Nasrallah ametoa wito kwa wote kunufaika na uzoefu wa nchi ambazo ziko mstari wa mbele kukabiliana na corona hasa Iran na China. Aidha amesema ni jukumu la kisheria la kila mtu kulinda maisha yake na ya familia haye na kila ambaye atazembea katika suala hili atakuwa ametenda dhambi kubwa.
Katibu Mkuu wa Hizbullah pia ameashiria hujuma ya ndege za kivita za Marekani dhidi ya vituo vya vikosi vya ulinzi vya Iran na kusema jinai hii ya Wamarekani haitabakia bila jibu.
Mapema Ijumaa, ndege za kivita za Marekani zilishambulia vituo vya Jeshi la Iraq na vikosi vya kujitolea vya wananchi wa Iraq maarufu kama Al Hashd al Shaabi katika mika ya Sallahudin, Babil, Basra na Karbala.
Katika hujuma hiyo maafisa watatu wa usalama wa Iraq waliuawa na wengine saba walijeruhiwa.