Katika mahojiano na IQNA, Sheikh Kharuddin al Hadi, mkuu wa Kituo cha Darul Quran kinachofungamana na Ofisi ya Mfawidhi wa Haram Takatifu ya Imam Hussein AS nchini Iraq amebainisha masikitiko yake kufuatia kuteketezwa moto nakala ya Qur'ani Tukufu nchini Sweden.
Amesema kitendo hicho kinaumiza zaidi wakati inapobainika kuwa baadhi ya maafisa wa serikali walikiunga mkono na hata polisi Sweden waliwapa ulinzi watenda jinai hiyo.
Rasmus Paludan, raia wa Denmark ambaye ni kinara wa chama chenye misimamo mikali cha Stram Kurs nchini Sweden aliteketeza moto nakala ya Qur'ani Tukufu katika mji wenye Waislamu wengi siku ya Alhamisi iliyopita.
Paludan, akiwa ameandamana na maafisa kadhaa wa polisi, alienda katika uwanja uliowazi katika mji wa Linkoping kusini mwa Sweden ambapo alitekeleza kitendo hicho kiovu. Pludan pia alikuwa amepanga kuteketeza nakala za Qur'ani katika miji kadhaa ya Sweden wakati wa siku kuu ya pasaka.
Sheikh Al Hadi amesema nchi za Magharibi na wale wote wanaodai kutetea haki za binadamu wameonyesha undumakuwili kwa kunyamazia kimya jinai hiyo kwa madai kuwa eti ni uhuru wa kujieleza
Harakati ya Hizbullah imeutaka Umma wote wa Kiislamu, Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu (OIC), Jumuiya ya Nchi za Kiarabu na mamlaka za kidini, taasisi za juu za Kiislamu, wanazuoni wa kidini, vyama na makundi ya kisiasa, na jumuiya zote za kimataifa na za kutetea haki za binadamu kuanzisha kampeni pana zaidi ya kulaani kitendo cha kuvunjiwa heshima Qur'an Tukufu nchini Sweden.