Kamati ya Quds (Jerusalem) na Msikiti wa Al-Aqsa ya Baraza la Wabunge la Palestina jana ilushutumu utawala ghasibu wa Israel kwa kujenga makaburi bandia karibu na Msikiti wa Al-Aqsa.
Kwa mujibu wa mkuu wa Kamati hiyo, Ahmad Abu Halabiyeh Mbunge, hili lilikuwa jaribio la kughushi "ushahidi" ili "kuthibitisha" uwepo wa kihistoria wa Wayahudi katika mji huu mtakatifu wa Palestina, Kiarabu na Kiislamu.
"Hivi karibuni, uvamizi wa Israel umejenga mamia ya makaburi ili kuthibitisha kuwepo kwa Wayahudi kulianza mamia ya miaka," alielezea Abu Halabiyeh. Takriban makaburi 300 ya bandia yamejengwa katika Jabal Al-Zaytoun, mashariki mwa Msikiti wa Al-Aqsa, alisema, na mengine 200 huko Wadi Al Hilwa eneo la Silwan, kusini mwa msikiti huo, pamoja na mamia zaidi katika maeneo tofauti katika Quds inayokaliwa kwa mabavu hasa katika Jiji la Kale.
Mbunge huyo alidokeza kuwa makaburi hayo yalijengwa katika kipindi cha miaka miwili iliyopita. Eneo moja, alisema, hata limeitwa "Makaburi ya Wayahudi".
"Huu ni upotoshaji wa wazi wa historia, pamoja na uthibitisho kwamba Waisraeli ni wavamizi," aliongeza Abu Halabiyeh. Kujenga makaburi bila mabaki ya binadamu ndani, alisisitiza, kunafanyika ili kuipa nguvu miradi ya ujenzi wa vitongoji haramu vya walowezi wa Kizayuni katika ardhi za Waplestina zinazoendelea kuporwa na utawala huo.
Aidha amesema uchokozi wa Israel dhidi ya Msikiti wa Al-Aqsa hutokea kila siku.
3481179