Taarifa zinasema mamia ya walowezi wa Israel kwa mara nyingine tena walivamia al-Aqsa chini ya ulinzi wa vikosi vya utawala katili wa Israel huo na kufanya vitendo vya uchochezi katika eneo hilo takatifu.
Katika taarifa iliyotolewa Jumapili, Idara ya Wakfu ya Kiislamu ya Jordan, ambayo inasimamia masuala ya Msikiti wa al-Aqsa ilisema wanajeshi wa Israel walifunga lango la Al Maghariba la Al Aqsa na kuwaruhusu Wayahudi 602 wenye itikadi kali kuingia ndani ya eneo hilo takatifu la Waislamu.
Vyombo vya habari vya Palestina viliripoti kwamba askari hao katili wa Israel waliwapiga waumini wa Kiislamu na waandishi wa habari waliokuwa wakiandika kuhusu yaliyojiri ndani na nje ya eneo takatifu la Quds Mashariki.
Wito wa kuwepo mara kwa mara kwa wanamgambo wa Kiyahudi wenye msimamo mkali katika Msikiti wa al-Aqsa umeongezeka katika siku za hivi karibuni sambamba na sikukuu za kuadhimisha sikukuu ya Kiyahudi.
Uvamizi wa walowezi wa Israel katika Msikiti wa al-Aqsa na ghasia dhidi ya Wapalestina zimekuwa zikiongezeka tangu baraza la mawaziri la siasa kali za mrengo wa kulia la Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu kuchukua madaraka mwezi uliopita wa Desemba.
Hii ni wakati ambapo ibada zisizokuwa za Kiislamu katika uwanja wa Msikiti wa al-Aqsa zimepigwa marufuku kwa mujibu wa makubaliano kati ya utawala unaoukalia kwa mabavu wa Israel na serikali ya Jordan kufuatia utawala huo wa Kiislam kuliteka eneo la Quds Mashariki kinyume cha sheria mwaka 1967.
Mnamo Mei 2022, jeshi katili la Israeli lilimpiga risasi mwandishi wa Al Jazeera Shireen Abu Akleh.
Mashirika ya kutetea haki za binadamu yamethibitisha kuwa ripota aliyeuawa wa Al Jazeera Abu Akleh alilengwa kimakusudi na wanajeshi wa Israel, na kutupilia mbali maelezo ya utawala wa Israel kwamba mauaji hayo hayakuwa ya kukusudia.
Abu Akleh alipigwa risasi kichwani na kuuawa na vikosi vya jeshi la Israel tarehe 11 Mei mwaka huo alipokuwa akifuatilia uvamizi wao katika kambi ya wakimbizi ya Jenin katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu. Wakati wa kuuawa kwake, mwanahabari huyo mwenye umri wa miaka 51 alikuwa amevalia mavazi ya vyombo vya habari yanayotambulika kwa urahisi.
Jeshi la Israel limeripotiwa kuwaua waandishi habari zaidi ya 55 katika ardhi ya Palestina inayokaliwa kwa mabavu tangu mwaka 2000.
3485398